OFISI YA RAIS
TAWALA ZA MIKOA NA IDARA MAALUM ZA SMZ

OFISI YA MKUU WA MKOA MJINI MAGHARIBI

Home>>Habari>>Maegesho ya Gari Michenzani Yazinduliwa
HabariHabari Mpya

Maegesho ya Gari Michenzani Yazinduliwa

Waziri wa  Habari Vijana Utamaduni na Michezo Mhe. Tabia Maulid Mwita amezindua rasmi maegesho ya gari  yaliyojengwa na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar (ZSSF), eneo la  Michenzani Mall.

Akihutubia mara baada ya uzinduzi huo  Waziri Tabia amewataka  ZSSF, Manispaa na Mkoa kuhakikisha eneo hilo lililojengwa kwa ajili ya maegesho ya gari na vyombo vya maringi mawili linatumika badala ya  watu kuegesha vyombo vyao barabarani.

Ameipongeza ZSSF kwa ujenzi wa mradi huo ambao amesema utapunguza tatizo la maegesho katika jengo la Michenzani Mall na kuwataka  kufikiria kujenga maegesho zaidi katika maeneo mbali mbali ya Mji.

Waziri Tabia ameitaka Wizara ya Nchi (OR) Fedha na Mipango kuendelea kushirikiana na ZSSF ili kutekeleza miradi mingine zaidi ambayo itarahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi wa Mkoa Mjini Magharibi na Zanzibar kwa ujumla

Naye Mhe. Sabiha Filifil Thani Mjumbe wa Kamati ya Uchumi ya Baraza la Wawakilishi akizungumza kwa niaba ya Kamati hiyo ameushauri Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar kutekeleza miradi yenye tija ili Mfuko huo uweze kujiendesha na kulipa mafao ya wastaafu.

Awali akizungumzia mradi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa ZSSF  Nassor Shaaban Ameir amesema maegesho hayo yana uwezo wa kuegesha gari sabini na tisa, vyombo vya maringi mawili, eneo kwa ajili ya watu wenye mahitaji maalum  na milango sita ya huduma za ATM.

Viongozi, wafanya kazi wa taasisi mbali mbali za Serikali pamoja na wananchi walihudhuria hafla hiyo ikiwa moja ya matukio ya Maadhimisho ya Kutimiza Miaka 59 ya Mapinduzi ya Zanzibar ambayo kilele chake kitafikia tarehe 12 Januari.