OFISI YA RAIS
TAWALA ZA MIKOA NA IDARA MAALUM ZA SMZ

OFISI YA MKUU WA MKOA MJINI MAGHARIBI

Home>>Habari>>Muungano umeleta mafanikio makubwa Mkoa Mjini Magharibi-RC
HabariHabari Mpya

Muungano umeleta mafanikio makubwa Mkoa Mjini Magharibi-RC

Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Mhe. Idrissa Kitwana Mustafa amesema Miaka 59 ya Muungano wa Tangayika na Zanzibar imeleta mafanikio na manufaa makubwa katika Mkoa wake.

Ameyasema hayo katika Sherehe za  Kilele cha Maadhimisho  ya Miaka 59 ya Muungano wa Tanzania zilizoadhimishwa Kimkoa katika viwanja vya Maisara, Wilaya ya Mjini.

Amesema moja ya mafanikio hayo ni uwepo wa hali ya amani na utulivu ambapo wananchi wa Mkoa huo wamekuwa wakifanya shughuli zao za kimaisha bila hofu na wasiwasi wowote kwa miaka yote 59 ya Muungano.

Ameeleza pamoja na amani na utulivu, Muungano umewanufaisha wananchi wa Mkoa wake kwa fursa mbali mbali zikiwemo fursa za ajira, elimu,  biashara  na nyenginezo ambazo zimekuwa zikiwapatia kipato mtu mmoja mmoja na pato la Serikali kupitia kodi zinazokusanywa.

Mkuu wa Mkoa ameeleza pia uwepo wa Taasisi za Muungano katika Mkoa huo zimesaidia sana kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi na kuzitaja  baadhi ya huduma hizo zikiwemo za kibenki, mawasiliano na afya.

Aidha Idrissa ameeleza kuwa kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii TASAF Mkoa wa Mjini Magharibi umenufaika na miradi mbali mbali ya maendeleo ngazi ya jamii pamoja na kuzisaidia kaya masikini kuweza kuinua kipato chao katika Shehia 121 za Mkoa huo.

Katika Sherehe hiyo, Mkuu wa Mkoa amewahimiza vijana kuendelea kuuenzi, kuulinda na kuutunza Muungano na kuachana na watu wanaoubeza Muungano kwa maslahi yao binafsi.

Akizungumza na hadhara iliyohudhuria maadhimisho hayo Professor Patrick Lumumba  amesema Watanzania wanapaswa kujivunia Muungano wao na kuhakikisha unaendelea kudumu kwa msalahi ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Naye Mkuu wa Wilaya Magharibi ‘A’ Suzan Peter Kunambi  ameeleza kwamba Muungano wa Tanyanyika na Zanzibar umeweza  kuondoa ubaguzi, ukabila, urangi na udini  na kuwaunganisha Watanzania kuwa wamoja.

Sherehe za Muungano hufanyika kila ifikapo April 26 ambapo kwa mwaka huu zimefanyika kimkoa  katika Mikoa yote ya Tanzania.